Waendesha mashtaka wa Kenya walisema Jumatatu waliidhinisha mashtaka ya mauaji dhidi ya watu sita, wakiwemo maafisa watatu wa polisi, kwa jukumu lao katika kumuua mwanablogu wa kisiasa ambaye kifo chake akiwa mikononi mwa polisi kilizua maandamano makubwa.
Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Kenya ilisema katika taarifa kwamba washukiwa hao sita watafikishwa mahakamani Jumanne.
Mmoja wa maafisa wa polisi alikuwa kamanda katika kituo alichozuiliwa Albert Ojwang, mwanablogu na mwalimu mwenye umri wa miaka 31, Nairobi.
Haijabainika mara moja iwapo washtakiwa hao waliwakilishwa na wakili.
Maelezo tata ya polisi
Ojwang alifariki mapema mwezi huu kufuatia kukamatwa kwake kama sehemu ya uchunguzi uliochochewa na malalamishi ya naibu mkuu wa polisi wa kitaifa, Eliud Lagat.
Lagat alikuwa amewasilisha malalamiko rasmi kuhusu madai ya uwongo na habari mbovu zilizochapishwa kumhusu kwenye mitandao ya kijamii, kulingana na shirika la polisi linalofadhiliwa na serikali.
Awali polisi walihusisha kifo cha Ojwang na kujitoa uhai lakini wakaomba msamaha baada ya uchunguzi wa maiti kubaini kuwa majeraha yake yalikuwa ni matokeo ya kushambuliwa.
Kifo cha Ojwang kilisababisha mamia kupinga ukatili wa polisi katika muda wa wiki mbili zilizopita.
Kulengwa maofisa wa chini pekee
Maandamano ya ziada yanatarajiwa siku ya Jumatano, ambayo pia yataadhimisha mwaka mmoja wa maandamano makubwa yaliyofikia kilele kwa kushambuliwa kwa bunge na vifo kadhaa kwa risasi za polisi.
Wanaharakati wa Kenya ambao wamekuwa wakipinga kifo cha Ojwang mara moja walishutumu waendesha mashtaka kwa kujihusisha na siri kwa kuwafungulia mashtaka maafisa wa ngazi ya chini pekee.
Lagat, ambaye amekana kufanya makosa yoyote, alijiuzulu kwa muda kutoka wadhifa wake wiki jana akisubiri kukamilika kwa uchunguzi wa kifo cha Ojwang.
Mmoja wa maafisa wengine walioshtakiwa kwa mauaji, James Mukhwana, aliwaambia wachunguzi kwamba wakuu wake walimwambia kulikuwa na "amri kutoka juu" ya kumtaka Ojwang adhulumiwe alipofika kituoni, kulingana na nakala ya ushahidi wake iliyoonekana na Reuters.
Reuters haijaweza kumfikia Lagat moja kwa moja kwa maoni yake na Huduma ya Kitaifa ya Polisi ilikataa kutoa maoni kwa niaba yake.