Jeshi la Somalia, likiungwa mkono na Vikosi vya Kusaidia na Kuimarisha Udhibiti wa Umoja wa Afrika nchini Somalia (AUSSOM), limevikomboa vijiji vya kimkakati vya Anole na Sabid kutoka kwa magaidi wa al-Shabaab baada ya karibu miezi miwili ya mapigano makali, afisa mkuu alisema Jumamosi.
Anole na Sabid, ziko katika jimbo la kusini-magharibi la Lower Shabelle, ni rasilimali za kijeshi za kimkakati na hutumika kama daraja muhimu.
Meja Jenerali Sahal Abdullahi Omar, kamanda wa jeshi la nchi kavu la Jeshi la Taifa la Somalia, aliviambia vyombo vya habari Jumamosi jioni kwamba operesheni ya "Silent Storm" ilisambaratisha wanamgambo wa al-Shabaab na kurudisha vijiji hivyo viwili.
Ukosefu wa usalama kwa muda mrefu
Alisema kundi la kigaidi lenye mafungamano na al-Qaeda liliripua daraja na miundo mingine, ikiwa ni pamoja na nguzo ya mawasiliano, kabla ya jeshi kutwaa tena vijiji hivyo.
Huu ni ushindi mkubwa wa kwanza wa jeshi la Somalia na walinda amani wa AU tangu al-Shabaab wachukue mji wa Adan Yabaal katika eneo la Shabelle ya Kati mwezi Aprili.
Kwa muda mrefu Somalia imekuwa ikikabiliwa na ukosefu wa usalama, huku makundi ya kigaidi ya al-Shabaab na ISIS (Daesh) yakiwa tishio kubwa zaidi.
Al-Shabaab imekuwa ikipigana na serikali ya Somalia kwa zaidi ya miaka 16 na mara nyingi huwalenga maafisa wa serikali na wanajeshi.