Mahakama ya Tunisia siku ya Ijumaa ilitoa hukumu ya kifungo cha miaka 22 jela bila kuwepo kwa Rais wa zamani Moncef Marzouki, mkosoaji mkali wa Rais Kais Saied, kwa tuhuma za kudhoofisha usalama wa taifa, na hivyo kuibua hofu ya upinzani ya kuongezeka kwa ukandamizaji dhidi ya wakosoaji.
Marzouki, ambaye alikuwa rais kuanzia 2011 hadi 2014, anamtuhumu Saied kwa kuanzisha utawala wa kimabavu baada ya kuliondoa bungeni na kutawala kwa amri tangu aliponyakua karibu mamlaka yote mwaka 2011.
Saied anatetea hatua zake kama hatua muhimu za kuleta utulivu wa Tunisia.
Huu ni uamuzi wa tatu dhidi ya Marzouki, baada ya mahakama kuamua mwaka jana kumfunga jela miaka minane na miaka minne kabla ya kesi hiyo katika kesi nyingine tofauti.
Demokrasia itarudi
Akizungumzia uamuzi huo, Marzouki alisema kutoka uhamishoni mjini Paris: "Ninawaambia majaji hawa: maamuzi yenu ni batili, na ninyi ni batili ... mtahukumiwa hivi karibuni".
"Demokrasia itarejea", aliongeza.
Mapema siku ya Ijumaa, mahakama nyingine ilimhukumu Sahbi Atig, afisa mkuu wa Ennahda, chama kikuu cha upinzani nchini humo, kifungo cha miaka 15 jela kwa tuhuma za utakatishaji fedha, wakili wake alisema.
Adhabu hiyo ya miaka 15 ilikuwa fupi kuliko hukumu zilizotolewa hivi majuzi. Mnamo Aprili, mahakama ilihukumu msururu wa viongozi wa upinzani, wafanyabiashara na mawakili kifungo cha hadi miaka 66 jela, kwa makosa ya kula njama.
Viongozi wengi wa vyama vya siasa nchini Tunisia wako gerezani, akiwemo Abir Moussi, kiongozi wa Chama Huru cha Katiba, na Rached Ghannouchi, mkuu wa Ennahda - wawili kati ya wapinzani mashuhuri wa Saied.