AFRIKA
2 dk kusoma
Rwanda imemkamata kiongozi wa upinzani Victoire Ingabire
Mwanasiasa wa upinzani wa Rwanda Victoire Ingabire anatuhumiwa kwa kujihusisha na vitendo vinavyochochea machafuko ya umma.
Rwanda imemkamata kiongozi wa upinzani Victoire Ingabire
Victoire Ingabire amekuwa na mzozo na serikali ya Rwanda kwa miaka mingi/ picha: AFP
20 Juni 2025

Rwanda imemkamata kiongozi maarufu wa upinzani Victoire Ingabire, ambaye anazuiliwa katika mji mkuu wa Kigali kwa tuhuma za kuchochea umma na kuunda shirika la uhalifu, shirika la uchunguzi la serikali lilisema.

Ingabire aliachiliwa huru mwaka wa 2018 baada ya kutumikia kifungo cha miaka sita jela kati ya miaka 15 aliyohukumiwa kutumikia mwaka 2012 kufuatia kukutwa na hatia kwa makosa ya kula njama ya kuunda kundi lenye silaha na kutaka kushusha hadhi mauaji ya kimbari ya mwaka 1994.

Sasa anashutumiwa kwa "kutekeleza jukumu la kuunda shirika la uhalifu na kujihusisha na vitendo vinavyochochea machafuko ya umma," Ofisi ya Upelelezi ya Rwanda ilisema katika taarifa yake siku ya Alhamisi. Haikusema ni lini atafikishwa mahakamani.

Kukanusha mauaji ya kimbari

Ingabire, ambaye anaongoza chama cha upinzani ambacho hakijasajiliwa cha DALFA–Umurinzi, alirejea kutoka uhamishoni Uholanzi ili kugombea nafasi ya urais katika uchaguzi wa rais mwaka 2010, lakini alizuiwa kugombea baada ya kushutumiwa kukana mauaji ya kimbari.

Pia alipigwa marufuku kugombea katika uchaguzi wa 2024. Mwaka jana Rais Paul Kagame, aliye madarakani kwa robo karne, alishinda tena uchaguzi baada ya kupata 99.18% ya kura, kulingana na chombo cha uchaguzi.

Kagame anasifiwa kwa kuibadilisha Rwanda kutoka magofu ya mauaji ya halaiki ya 1994 hadi kuwa uchumi unaostawi lakini sifa yake pia imechafuliwa na shutuma za muda mrefu za ukiukwaji wa haki na kuunga mkono waasi katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Rwanda inakanusha madai hayo.


CHANZO:TRT Afrika and agencies
Kionjo cha TRT Global. Tupe mrejesho wako.
Contact us