Hadi sasa hakuna ongezeko la uhamiaji wa kinyume cha sheria kufuatia mapigano kati ya Israel na Iran, Wizara ya Ulinzi ya Kitaifa ya Uturuki ilisema Alhamisi.
Jeshi la Uturuki litaendelea kuchukua hatua zote muhimu za kiusalama dhidi ya uwezekano wa kuzuka kwa wimbi la uhamiaji, msemaji wa wizara hiyo Zeki Akturk alisema.
Katika wiki moja pekee iliyopita, magaidi watano wa kundi la PKK waliokimbia maficho kaskazini mwa Iraq na Syria wamejisalimisha, Akturk aliwaambia waandishi wa habari katika mji mkuu wa Ankara.
Aliongeza kuwa idadi kubwa ya silaha, risasi na vifaa mbalimbali vilikamatwa katika mapango, makazi na maficho ya magaidi katika Operesheni Claw-Lock na maeneo mengine ya operesheni, na hivyo kusababisha silaha hizo kutoweza kutumika.
Akturk alisema kuwa Jeshi la Uturuki linaendelea na operesheni zao, ikiwa ni pamoja na misako na shughuli za usalama wa mpaka ili kuhakikisha amani, usalama na utulivu wa nchi.
Magaidi wa PKK mara kwa mara hujificha kaskazini mwa Iraq, karibu na mpaka wa Uturuki, kupanga mashambulizi katika ardhi ya Uturuki.
Katika miaka ya hivi karibuni, Uturuki imefanikiwa kuwashinda magaidi wa PKK ndani na nje ya nchi, huku idadi inayoongezeka ya wanachama wa PKK wakiacha kundi la kigaidi na kujisalimisha kwa vikosi vya Uturuki. Waasi kama hao wanaweza kufaidika na sheria ya adhabu ya Uturuki.
Katika kampeni yake ya takriban miaka 40 ya ugaidi dhidi ya Uturuki, PKK- iliyoorodheshwa kama shirika la kigaidi na Uturuki, Marekani, na EU-imehusika na vifo vya zaidi ya watu 40,000, ikiwa ni pamoja na wanawake na watoto.
Israel inaendesha machafuko katika eneo
"Mazungumzo yalipokua yakiendeleai kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran, Israel imeanzisha mashambulizi kinyume cha sheria dhidi ya jirani yetu Iran, kwa mara nyingine tena kuhatarisha utulivu na amani ya kikanda," Akturk alisema.
Akilaani mashambulizi ya Israel yaliyolenga Iran, alibainisha kuwa Israel imeipuuza sheria za kimataifa katika mashambulizi yake ya hivi karibuni huko Gaza, Lebanon, na sasa Iran inafichua wazi nia yake ya kuzidisha mizozo.
Alisema kuwa uchochezi wa Israel, ambao haujui mipaka, unaingiza eneo hilo katika machafuko na lazima ikomeshe mara moja mashambulizi yake, yanayosababisha kukosekana kwa utulivu katika eneo jirani.
"Israel lazima ikomeshe mara moja matamshi ya uchokozi na mashambulizi ambayo yatazidisha mzozo," vyanzo vya Wizara ya Ulinzi ya Uturuki pia vilisema, vikiashiria mzozo unaoendelea kati ya Israel na Iran.
Duru hizo zilisema ripoti za ndege za Israel kukiuka anga ya Uturuki katika siku ya kwanza ya mashambulizi ya anga dhidi ya Iran si sahihi, na kusisitiza kwamba tangu awali, harakati zote za anga zilifuatiliwa kwa karibu.
Kuhusu uwezekano wa ukiukaji wa anga wa ndege za Israel, ndege za tahadhari zilipaa na kuanza misheni ya doria ndani ya anga ya Uturuki, vyanzo viliongeza.
Vyanzo hivyo vilisisitiza kwamba kwa baada ya kuanza tu kwa mashambulizi ya anga ya Israel, hatua za kulinda "anga na mipaka yetu zimeimarishwa."
"Sera za uchokozi za Israel dhidi ya Gaza, Lebanon, Syria, na Iran zinavuruga zaidi utulivu ambayo tayari ni dhaifu katika eneo hilo," vyanzo viliongeza.
Vikosi vya Wanajeshi wa Uturuki, moja ya jeshi la kisasa zaidi, linaloheshimika na lenye nguvu zaidi ulimwenguni, bado linaweza kulinda nchi na watu wake sasa na katika siku zijazo, vyanzo viliongeza zaidi.
Ulinzi wa anga wa Uturuki
Vyanzo vya wizara hiyo vilisema kuwa juhudi za kudumisha ulinzi wa anga na makombora wa Uturuki kama mfumo wa tabaka nyingi na mpana zinaendelea.
Mbali na mifumo ya ndani ya rada na ulinzi wa anga, kazi inaendelea kuimarisha uwezo wa udhibiti.
Hatua zimewekwa kuhakikisha vitengo vya ulinzi wa anga na mifumo ya silaha inasalia katika kiwango cha juu cha utayari, vyanzo viliongeza.
Zikieleza kuwa Vikosi vya Wanajeshi wa Uturuki viko kazini wakati wote na teknolojia ya hali ya juu na wafanyikazi kulinda mipaka ya Uturuki, vyanzo vilisisitiza kuwa hakuna harakati za uhamiaji zisizodhibitiwa, na madai hayo ni ya kupotosha na kwamba hakuna data au uthibitisho rasmi wa uhamiaji wowote wa watu wengi kuingia nchini.
Uwezo wa Uturuki wa kuhakikisha usalama wa mpaka na kukabiliana na majanga ya kibinadamu yanayoweza kutokea unadumishwa kwa kiwango cha juu zaidi kwa uratibu na taasisi husika za serikali, vyanzo vya wizara vilisisitiza.
"Uturuki inafanya kazi kwa njia iliyodhibitiwa na yenye utaratibu kama nchi inayounga mkono utulivu wa kikanda na kutekeleza majukumu yake ya kibinadamu," vyanzo viliongeza.