Ofisi ya Upelelezi ya Rwanda (RIB) imesema kuwa Wanyarwanda 105 walirejeshwa makwao katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita baada ya kuwa waathirika wa biashara haramu ya binadamu.
Urejeshwaji huo ulifanyika kati ya Juni 2024 na Mei 2025.
“Takwimu za RIB zinaonyesha kuwa kuanzia Juni 2019 hadi Julai 2024, watu 39 walinaswa walipokuwa njiani kusafirishwa. Zaidi ya hayo, kati ya Julai 2024 na Machi 2025, baadhi ya 57 walinaswa kabla ya kuondoka nchini, ambayo ilihusisha kesi 24.” msemaji wa RIB Thierry Murangira aliwaambia waandishi wa habari.
Wanyarwanda 10 walirejeshwa mnamo Aprili 23, ambao walikuwa wamesafirishwa kwenda Myanmar.
"Waathiriwa hawa walishawishiwa na ahadi za kazi zenye malipo mazuri," Murangira alisema.
Walikuwa wameahidiwa kazi zenye malipo makubwa katika vituo vya kupiga simu, huku mishahara ikiwa kati ya $1,000 na $1,500.
Hata hivyo, badala yake walifanyishwa kazi ngumu na vitendo vya ulaghai.
"Waliambiwa kwamba kadiri wanavyofanya kazi kwa bidii, ndivyo wangepata pesa nyingi zaidi. Lakini yote yalikuwa ni mtego."
"Wasafirishaji haramu wa binadamu huwapa watu matumaini kwa kutoa viza bandia, ufadhili wa masomo, au ajira," Murangira alisema.
"Mara nyingi wanafanya kazi kupitia mitandao ya kijamii, mashirika ambayo hayajasajiliwa, au watu binafsi wanaojifanya watu wema."
Kulingana na RIB mara nyingi waathiriwa hudhulumiwa kupitia kazi za kulazimishwa, ukahaba, ulanguzi wa viungo, au uhalifu wa kulazimishwa, kama ilivyokuwa kwa baadhi ya vijana wanaosafirishwa kwenda Myanmar.
"Usafirishaji haramu wa binadamu unageuza watu kuwa bidhaa. Ni ukiukwaji mkubwa wa utu," Murangira ameongezea.
Serikali ya Rwanda imesema inafanya kazi kwa karibu na nchi zinazotambuliwa kuwa ni sehemu za mara kwa mara za Wanyarwanda kusafirishwa, na kushinikiza kufunguliwa mashitaka kwa wasafirishaji haramu na kusambaratisha mitandao ya magendo.
Shida hii ipo kwa nchi tofauti barani.
Aprili 2025 serikali ya Kenya ilifanikiwa kuwarejesha nyumbani raia 153 ambao walisafirishwa kwenda kwenye makazi ya kitapeli nchini Myanmar.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Masuala ya Diaspora Roseline Njogu alisema watu hao waliingizwa nchini Myanmar kwa kisingizio cha uwongo cha ajira na kazi zenye faida kubwa, na kukumbana na kazi ya kulazimishwa na unyonyaji baada ya kunaswa katika shughuli za ulaghai.