Wizara ya Afya ya Sudan Jumatatu iliripoti kupungua kwa vifo vya kipindupindu katika Jimbo la Khartoum.
Taarifa ya Wizara ya Afya nchini humo imesema kuwa maambukizi 605 ya kipindupindu, pamoja na vifo sita, vilisajiliwa katika jimbo hilo Jumapili, kutoka kwa vifo 12 siku moja kabla.
Wizara hiyo ilisema maambukizi hayo mapya yalirekodiwa katika miji ya Karrari, Omdurman na Ombada katika jimbo hilo.
Kulingana na taarifa za Wizara, ongezeko la vituo vya afya vilivyopo nje ya miji, wafanya usafi wa mazingira, na afua za afya miongoni mwa jamii zilizoathiriwa ziliongeza viwango vya kupona na kupunguza maambukizi.
Siku ya Alhamisi, Wizara iliripoti maambukizi mapya 1,375 ya kipindupindu na vifo 23 huko Khartoum, pamoja na maambukizi 2,729 na vifo 172 kote nchini. Mnamo Agosti 2024, mamlaka ya Sudan ilitangaza kipindupindu kuwa janga la kitaifa.
Miundombinu ya afya ya Sudan imekuwa moja ya iliyoathiriwa zaidi na vita vya wenyewe kwa wenyewe vinavyoendelea kati ya jeshi la Sudan na Kikosi cha RSF, ambacho kimekuwa kikitokea tangu Aprili 2023.