Bara la Afrika lazima liimarishe upatikanaji wa chanjo zao wenyewe ili liweze kukabiliana na maradhi, Rais wa Angola amesema katika kikao cha dharura siku ya Jumatano kuhusu mlipuko wa kipindupindu ambao umewaua watu zaidi ya 700 nchini Angola mwaka huu pekee.
Rais Joao Lourenco, mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika, amehutubia kikao cha viongozi wa Afrika kwa njia ya video kuhusu kuongezeka kwa maambukizi ya kipindupindu katika mataifa kadhaa, ofisi yake ilisema.
"Ili kuhakikisha tunakuwa tayari kikamilifu kwa ajili ya matukio ya baadaye, ni muhimu kuwa na dawa na uzalishaji wa chanjo katika bara letu," Lourenco alisema, kulingana na taarifa iliyosambazwa katika mitandao ya kijamii.
"Kutegemea tu misaada kutoka nje inakwamisha uwezo wetu wa kudhibiti afya zetu," alisema katika mkutano huo uliohudhuriwa na mkuu wa Shirika la Afya Duniani Tedros Adhanom Ghebreyesus.
Chanjo zaidi ya 90% zinazotumika Afrika zinaagizwa kutoka nje
Chanjo zaidi 90%, dawa, vifaa vya kupima vinavyotumika kote barani vinatoka nje ya bara la Afrika, Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia magonjwa barani Afrika (CDC) kimesema katika ripoti yake mwezi Aprili.
Nchi kadhaa barani Afrika zinakabiliana na mlipuko wa kipindupindu – huku Sudan, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Angola zikiathirika zaidi.
Angola ilikuwa na maambukizi zaidi ya 24,530 mwaka huu na kufikia tarehe 2 Juni watu 718 walikuwa wamefariki, taarifa hiyo ilisema.
Vifo zaidi 170 vimetokana na kipindupindu Sudan kwa wiki moja
Tarehe 27 Mei wizara ya afya ya Sudan ilisema kuwa kulikuwa na vifo 172 ndani ya wiki moja katika nchi hiyo iliyokumbwa na vita.
Ripoti ya CDC imesema Afrika imekuwa na matatizo kwa sababu imekuwa ikitegemea mataifa ya nje wakati wa milipuko mibaya, ikiwemo UVIKO-19, Ebola, Marburg na mpox.