Jeshi la Sudan limetangaza siku ya Jumatano kuwa vikosi vyake vimechukuwa tena udhibiti wa jimbo la Blue Nile kusini mashariki mwa nchi kufuatia makabiliano dhidi ya wapiganaji wa Rapid Support Forces (RSF) na Sudan People’s Liberation Movement–North (SPLM-N).
“Wanajeshi wetu wamefanikiwa kuingia eneo la Baldagu na sehemu za karibu katika jimbo la kusini la Blue Nile na kuondoa wapiganaji wa RSF na SPLM-North,” msemaji wa jeshi Nabil Abdullah alisema katika taarifa.
Hakujakuwa na majibu kutoka kwa RSF au SPLM-North kuhusu taarifa hiyo ya jeshi.
Jeshi linadhibiti maeneo mengi jimbo la Blue Nile, ambapo limekuwa likipigana na vikosi vya SPLM-North tangu 2011. Waasi hao wanataka utawala wao wenyewe katika majimbo ya Blue Nile na Kordofan Kusini.
Katika taarifa tofauti, jeshi linasema limepiga “kundi kubwa” la wapiganaji wa RSF huko Dilling, mji wa pili kwa ukubwa katika jimbo la Kordofan Kusini.
Jeshi limesambaza video katika ukurasa wake rasmi wa Facebook, ambayo linasema inaonyesha wakazi wa Dilling wakisherehekea pamoja na wanajeshi wa Sudan.
Wapiganaji wa RSF na jeshi wamekuwa wakipigana vita vikali wakitaka udhibiti wa nchi tangu Aprili 2023, na kusababisha mauaji ya maelfu ya watu na kufanya Sudan kuwa na hali mbaya zaidi kwa watu duniani. Maelfu ya watu wameuawa na mamilioni kuondolewa katika makazi yao.