ULIMWENGU
5 dk kusoma
Muislamu Muarabu na Mkristo Mzungu: Nani hupewa jina la gaidi?
Muingereza mzungu alipowagonga kwa gari waliokuwa wakisherehekea ushindi wa Liverpool, mamlaka ilikanusha ugaidi, licha ya watu zaidi ya 100 kujeruhiwa. Kwa nini tukio hilo hilo huchukuliwa tofauti iwapo mhalifu si Mzungu au ni Muislamu?
Muislamu Muarabu na Mkristo Mzungu: Nani hupewa jina la gaidi?
Mwezi uliopita, zaidi ya watu 100 walijeruhiwa wakati wa kusherehekea ushindi wa Liverpool, katika shambulio la makusudi. / Reuters
11 Juni 2025

Baada ya tukio la gari lililosababisha vurugu wakati wa sherehe za ushindi wa klabu ya Liverpool katika Ligi Kuu ya England—tukio ambalo lilisbaabisha watu 109 kujeruhiwa, majeruhi mdogo zaidi akiwa na umri wa miaka 9 na mkubwa zaidi akiwa na miaka 78—polisi walichukua hatua isiyo ya kawaida.

Ndani ya saa chache, walimtaja mshukiwa: Paul Doyle, mwanaume Muingereza mzungu mwenye umri wa miaka 53 kutoka eneo la West Derby.

Miongoni mwa Waislamu wa Uingereza, kulikuwa na afueni. Ukweli mchungu ni huu: kama mshambuliaji angekuwa Muislamu, au hata mwenye asili ya Asia, vichwa vya habari vingekuwa tofauti kabisa, na kungekuwa na athari kwa jamii.

Tumewahi kuona hili katika siku za nyuma. Mnamo Agosti 2024, ripoti za uongo zilizoeleza kuwa mshukiwa wa tukio la uchomaji visu huko Southport alikuwa mhamiaji au Muislamu zilisababisha ghasia kote Uingereza. Biashara zinazomilikiwa na Waislamu zililengwa. Hoteli zinazowahifadhi wahamiaji zilishambuliwa.

Na yote haya yalitokana na taarifa potofu ambazo mamlaka zilishindwa kuzikanusha kwa haraka. Mshambuliaji, ilibainika, hakuwa mhamiaji wala Muislamu. Lakini madhara yalikuwa tayari yamefanyika.

Utambulisho wa mapema wa mshukiwa, hasa ukijumuisha kabila lake, huenda ulikuwa jaribio la kuzuia uvumi mtandaoni, ambao unaweza kuenea haraka na kusababisha taarifa potofu za hatari.

Hata hivyo, polisi walikuwa wazi kuhusu jambo moja: licha ya walioshuhudia kuripoti tukio hilo kuwa la makusudi, tukio hilo halikuchukuliwa kama kitendo cha ugaidi.

Doyle sasa ameshtakiwa kwa makosa kadhaa, yakiwemo kuendesha gari kwa hatari na nia ya kusababisha madhara makubwa kwa watu. Lakini si ugaidi.

Hii ndiyo sababu uamuzi wa kumtaja mara moja Paul Doyle—Muingereza mzungu —ulikuwa wa maana. Ni wazi, polisi wanajifunza kutokana na makosa yao ya awali. Labda wanaanza kutambua kuwa ukimya na kuchelewa kunachochea taarifa za hatari.

Hata hivyo, swali linabaki: kwa nini mtu kama Doyle, ambaye inadaiwa aliamua kwa makusudi kuendesha gari kuelekea kuliko umati, hachukuliwi kama gaidi?

Sheria ya Ugaidi ya Uingereza ya mwaka 2000 inatoa ufafanuzi wazi. Ugaidi unajumuisha matumizi au tishio la vurugu kubwa dhidi ya watu, uharibifu wa mali, au vitendo vinavyohatarisha maisha au usalama wa umma, vinapofanywa kwa lengo la kushawishi serikali, kutisha umma, au kuendeleza sababu ya kisiasa, kidini, kikabila, au kiitikadi.

Lakini mara kwa mara, sheria hii inaonekana kutumika kwa upendeleo.

Tumeona kesi ya Salih Khater. Mnamo Agosti 2018, aliendesha gari kuelekea sehemu ya watembea kwa miguu nje ya Majengo ya Bunge huko Westminster, London. Alikamatwa haraka, akazuiliwa chini ya Sheria ya Ugaidi, na kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani. Hakuwa na uhusiano na mashirika ya kigaidi.

Msikiti wa Kati wa Birmingham ulithibitisha kuwa hakuwa anajulikana kufanya ibada zake hapo na hakuonyesha dalili za msimamo mkali. Lakini hakuwa mzungu, mkimbizi kutoka Sudan aliyekuwa raia wa Uingereza. Hilo lilitosha.

Kitendo cha Khater kilifanana na cha Doyle kwa vurugu na uzembe wake. Lakini wakati Khater alibandikwa jina la gaidi, Doyle anachukuliwa kama mhalifu wa kawaida, asiyehusishwa na itikadi yoyote, ugonjwa wa akili, au tatizo la kijamii.

Kwa hivyo, ni nini kinachoendelea?

Siasa za utambulisho

Haiwezekani kupuuza jinsi utambulisho wa mshambuliaji—kabila lake, dini, tabaka lake, na utaifa wake—unavyoathiri si tu taarifa za vyombo vya habari bali pia maneno yanayotumika kuelezea uhalifu.

Utambulisho wa Muingereza mzungu hauleti tu aina fulani ya upendeleo wa kijamii na kisiasa bali pia kinga ya namna taarifa zinavyowasilishwa. Mara tu maneno hayo yanapotamkwa, vyombo vya habari, umma, na polisi kwa pamoja huonekana kubadilika na kutumia lugha laini: matumizi ya dawa za kulevya, matatizo ya afya ya akili (Doyle ni mwanajeshi wa zamani), matukio yasiyofungamana na kundi lolote.

Lakini ikiwa watu 109 wanadhuriwa kwa makusudi, wakiwemo watoto, je, hilo si ugaidi? Je, wale waliopataikana na kadhia hiyo hawakutishwa?

Ukweli ni kwamba, neno gaidi limekuwa na mwelekeo wa kibaguzi, ugaidi mara nyingi huelezwa kama ugaidi wa Kiislamu. Linakuwepo tu pale mshambuliaji anapokuwa si mzungu, Muislamu, mzaliwa wa kigeni, au yote matatu.

Wakati huo huo, wanaume wazungu wenye vurugu mara chache, ikiwa ni mara chache sana, huelezwa kwa kutumia neno hilo, hata pale vitendo vyao vinapolingana na ufafanuzi wa kisheria.

Upendeleo huu haupotoshi tu uelewa wetu wa ugaidi, bali pia ni hatari. Kwa kuonyesha ugaidi kama kitu kinachofanywa tu na Waislamu, tishio linalokuwa la vurugu za mrengo wa kulia linafichwa.

Kinachofuata ni hatari zaidi. Wale walioko pembezoni—Waislamu, wahamiaji, jamii za watu wa rangi—wanazidi kunyooshewa vidole, wakilazimika kubeba mzigo wa hatia ya pamoja kwa uhalifu ambao hawakufanya. Na wahalifu wazungu? Wanabaki kuwa wa kawaida tu, uhalifu wao ukichukuliwa kama kushindwa binafsi, si vitisho vya mfumo.

Kutokuwepo kwa usawa katika lugha na majibu si tu kunakatisha tamaa, bali pia ni hatari. Kunapotosha mtazamo wa umma kuhusu nini ugaidi, na muhimu zaidi, nani anaweza kuwa gaidi. Kunaruhusu jamii nzima kulaumiwa huku nyingine zikibaki salama.

Lugha ni muhimu. Maneno tunayoyatumia huunda mfumo wa haki, huathiri hisia za umma, na kutoa dira ya sera za kisiasa. Kukataa mara kwa mara kuita vurugu za wazungu ugaidi kunatoa ujumbe wa kutisha: ni maisha ya baadhi ya watu tu yanayostahili kuchukuliwa kwa hasira. Ni matukio fulani tu yanayostahili kuchukuliwa kwa uzito kamili wa sheria.

Hatuhitaji watu zaidi kuitwa magaidi. Neno hilo lina athari kubwa. Lakini tunahitaji usawa ili neno hilo lisigeuzwe kuwa chombo cha ukandamizaji, linalotumiwa tu dhidi ya makundi fulani.

Ikiwa ugaidi unatakiwa kuwa na maana yoyote, lazima utumike kwa wote wanaofanya vitendo vya kigaidi, si tu wale wanaoonekana kufanana na dhana hiyo. Vinginevyo, si haki tunayolinda, bali ni upendeleo na ubaguzi uliofunikwa kwa lugha ya kisheria.

Kwa hivyo, hebu tujiulize: ugaidi ni kuhusu kile unachofanya, au wewe ni nani?

Mpaka tujibu hilo kwa ukweli kabisa, mfumo wa haki utaendelea kuwa hatari kama ulivyo na upendeleo.

Kionjo cha TRT Global. Tupe mrejesho wako.
Contact us