Kulingana na mashuhuda ambao hawakutaka kutajwa majina yao tukio hilo lilitokea siku ya Jumatatu, kufuatia tuhuma zilizotolewa na wanachama na sehemu ya kikundi cha chama tawala nchini Burundi, kijulikanacho kama Imbonerakure.
Umoja wa Mataifa na wanaharakati wa haki za kibinadamu, wanakitambua kikundi hicho kama wanamgambo.
"Kikundi cha vijana wa Imbonerakure kilivamia nyumba za watu 10 wanaoshukiwa kuwa ni washirikina na kuanza kuwashambulia," alisema mmoja wa mashuhuda.
"Watu sita waliuwawa, huku wawili wakichomwa moto wakiwa hai. Wengine walipigwa na mawe makubwa vichwani," aliongeza.
Hadi kufikia sasa, watu 12 wanashikiliwa na polisi kuhusiana na tukio hilo, kwa mujibu wa gavana wa Bujumbura Desire Nsengiyumva.
Vikundi mbalimbali vya haki za kibinadamu, ikiwemo Human Rights Watch, vimekituhumu kikundi cha Imbonerakure kwa utesaji na mauaji ya watu, hususani wakati wa utawala wa aliyekuwa rais wa Burundi Pierre Nkurunziza, aliyeongoza nchi hiyo kati ya 2005 na 2020.