Naibu Rais wa zamani wa Kenya Rigathi Gachagua amebadilisha msimamo wake mahakamani na sasa anataka kulipwa fidia badala ya kurejeshwa katika ofisi ya kiongozi wa pili wa taifa.
Gachagua anasema kura aliyopigiwa na bunge ya kutokuwa na imani naye ilikuwa ‘‘kinyume na sheria’’
Siku ya Alhamisi mawakili wake wakiongozwa na mwanasheria mwandamizi Paul Muite waliwasilisha maombi mahakamani ya kutaka kubadilisha malalamiko yao kutoka kwa kurejeshwa ofisini hadi kulipwa fidia.
‘‘Mlalamikaji anaomba kupinga kuondolewa kwake madarakani na angeomba kubadilisha shauri lake. Angependa alipwe fidia ya fedha ambazo angelipwa kama angekuwepo kwa kipindi chake chote cha miaka mitano,’’ Muite alifahamisha mahakama.
Hatua hii inaonesha kubadilika kwa msimamo wa Gachagua ambao awali alitaka arejeshwe ofisini.
Wanasheria wake waliweka wazi kuwa kwa sasa hawana haja tena ya kutaka mteja wao arejeshwe madarakani kama Naibu Rais na badala yake wanachotaka ni kulipwa fidia.