Aliyekuwa Waziri Mkuu wa Kenya, Raila Odinga, amelaani vikali matamshi ya Waziri wa Mambo ya Ndani, Kipchumba Murkomen, akisisitiza kuwa polisi hawana ruhusa ya kuua na kwamba kauli kama hizo zinavunja misingi ya utawala wa sheria na kudhihirisha kutothamini maisha ya binadamu.
"Kamwe polisi wasifyatue risasi kwa lengo la kuua. Polisi hawana leseni ya kuua. Iwapo mtu ametenda uhalifu, akamatwe na afikishwe mahakamani ili ajibu mashtaka dhidi yake," alisema Raila.
Matamshi haya ya Raila yamekuja kufuatia wito wa Murkomen kwa polisi "kummaliza" mtu yeyote anayekaribia kituo cha polisi kwa nia isiyojulikana, kauli iliyozua taharuki mitandaoni na katika duru za kisiasa.
Hata hivyo, Murkomen amejitetea, akisema maneno yake yalinukuliwa nje ya muktadha. Alifafanua kuwa alikuwa akirejelea Kifungu cha 61(b)(i) cha Sheria ya Huduma ya Polisi ya Kitaifa, ambacho kinawaruhusu maafisa wa polisi kutumia silaha za moto kujilinda au kuwalinda wengine dhidi ya vitisho vya kifo au majeraha makubwa.