Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat amejiondoa katika majukumu yake ili kupisha uchunguzi kuhusu kifo cha Albert Ojwang.
Katika taarifa yake ya Juni 16, 2025, Lagat alisema hatua hiyo ilikuwa katika "mawazo mazuri na makini" kuhusu majukumu yake.
Alitaja uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha Albert Ojwang, aliyekufa akiwa chini ya usimamizi wa polisi, kuwa sababu ya kuondoka ofisini kwa muda.
"Leo nimechagua kujiuzulu ... nikisubiri kukamilika kwa uchunguzi," alisema.
Baadhi ya Wakenya wamemnyooshea kidole Lagat ikidaiwa kuwa Ojwang’ alikamatwa kufuatia malalamishi ya naibu huyo aliyemshtumu kwa kumharibia jina kwenye mitandao ya kijamii.
Wakenya waliandamana Jumanne wiki iliyopita wakitaka ajiuzulu huku uchunguzi ukiendelea.

Lagat aliongeza kuwa naibu wake atafanya kazi za ofisi hiyo hadi uchunguzi utakapokamilika. Alionyesha nia ya kuunga mkono mchakato wa uchunguzi na akatuma risala za rambirambi kwa familia ya Ojwang.
Ojwang alifariki baada ya madai ya kushambuliwa akiwa kizuizini katika Kituo Kikuu cha Polisi, Nairobi.
Kesi hiyo imezua hasira kwa umma na kupelekea kukamatwa kwa OCS wa kituo hicho, Samson Talam.
Uchunguzi unaendelea, ukiongozwa na Mamlaka Huru ya Kusimamia Polisi (IPOA).