Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama Cha Wakulima (AAFP) Kunje Ngombale Mwiru, ameahidi kujenga bwawa la mamba Ikulu, iwapo Watanzania watampa ridhaa ya kuiongoza nchi hiyo.
Akizungumza jijini Morogoro hivi karibuni wakati wa kampeni za kunadi sera zake, Mwiru amesema kuwa kuwa analenga kupambana na mafisadi, ikiwemo kupambana na kukomesha vitendo vya kifisadi nchini Tanzania.
“Ndugu zangu, kiama cha mafisadi kinakuja. Mkinachagua tarehe 29, Ikulu yangu kutakuwa na bwawa la kufuga mamba. Ikulu yangu itakuwa na bwawa la kufuga mamba. Huyo mamba ni kwa ajili ya kitanzi cha mafisadi,” alibainisha.
Kulingana na Mwiru, yeyote atakayefanya vitendo vya kifisadi, ataenda kukutana na mamba kwenye ikulu yake, akiahidi kumtumbukiza yeyote atakayejihusisha na ufisadi na uhujumu uchumi ndani ya bwawa hilo.
“Kama umewatesa Watanzania wenzako kwa muda mrefu, mtu anakula pesa za zahanati 5, zahanati 6, leo mnamwacha anatembea, eti anavinjari mtaani, atakutana na kitanzi cha Rais. Ni lazima nitamdumbukiza kwenye bwawa la mamba, apambane na mamba,” aliongeza.
Kwa mujibu wa Tume Huru ya Uchaguzi Tanzania (INEC), jumla ya vyama vya siasa 18 vitashiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, huku vyama 17 vikisimamisha wagombea Urais.