Mgombea Urais wa Jamuhuri ya muungano wa Tanzania kupitia chama cha wananchi (CUF) Gombo Samandito Gombo amesema serikali yake itaboresha maslahi ya wafanyakazi ili wapunguze makali ya maisha wanayokumbana nayo.
Akizungumza wakati wa kampeni zake katika kata ya Katoro wilayani Bukoba mkoani Kagera, Gombo alisema kuwa chama chake kitahakikisha kinaboresha maslahi ya wafanyakazi ili wapunguze makali ya maisha, hususani yale yaliyosababishwa na uchukuaji holela wa mikopo.
“Sisi CUF tunasema haya maumivu ya maisha waliyo nayo wafanyakazi wetu mpaka ikafika mahali hawatuhudumii vizuri lazima na yenyewe kwa kutumia kodi zetu tuwape wanachostahili ilo waweze kutuhudumia vizuri, "alisema mgombea huyo wa Urais.
Kulingana na Gombo, chama chake kimeazimia kuboresha mishahara ya wafanyakazi pamoja na kuwajengea nyumba ili waweze kukaa sehemu nzuri na kufanya kazi kwa utulivu wa akili, bila kujihusisha na rushwa ndogo ndogo kwa wananchi.
Mbali na hayo, Gombo aliongeza kuwa iwapo watapata ridhaa ya kuiongoza Tanzania, watahakikisha kwamba kila mwisho wa mwezi wazee wote wanapata posho kama ambavyo wanapata wastaafu waliofanya kazi serikalini.