Mamlaka hizo zimesema kuwa angalau Wapalestina 20, wakiwemo wanahabari watano na mtu mmoja wa zima moto, waliuawa na wengine kujeruhiwa Jumatatu katika shambulio la Israeli dhidi ya hospitali ya Nasser huko Khan Younis.
Waliouawa pia ni pamoja na Hussam Al Masri, aliyekuwa mtaalamu wa picha wa shirika la habari la Reuters; Mariam Abu Daqqa, aliyekuwa mwandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vya habari ikiwemo The Independent Arabic na shirika la habari la The Associated Press; Ahmed Abu Aziz kutoka Quds Feed Network, Mohammed Salama wa Al Jazeera na Moaz Abu Taha wa Reuters.
Kwa mujibu wa Anadolu, jeshi la Israeli lililenga ghorofa ya juu ya jengo la dharura linalojulikana kama "ghorofa ya Al-Yassin."
Mamlaka za Gaza zimesema jeshi la Israeli lilipiga makombora mara mbili ghorofa ya nne ya jengo la hospitali, huku shambulio la pili likitokea wakati timu za uokoaji zilipofika kuwahifadhi majeruhi na kuondoa maiti.
Katika shambulio jingine dhidi ya wanahabari, mwandishi wa habari wa Palestina Hassan Douhan aliuawa na jeshi la Israeli huko Khan Younis, na kufikisha idadi ya wanahabari waliouawa Jumatatu kuwa sita.
Nchi kadhaa, mashirika ya haki za binadamu, Umoja wa Mataifa, Shirika la Ushirikiano wa Mataifa ya Kiislamu (OIC) na mashirika ya habari wamekasirika na kulaani shambulio la Israel.
Uturuki
Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan alilaani shambulio la Israeli, akisema serikali ya waziri mkuu wa Israeli Netanyahu inaendelea kwa ukatili bila huruma kuharibu kila kitu kinachohusiana na ubinadamu.
Ofisi ya mawasiliano ya rais wa Uturuki ilisema mashambulio ya hivi karibuni ya Israel Gaza ni “shambulio dhidi ya uhuru wa waandishi wa habari na uhalifu mwingine wa kivita.”
“Israel, ambayo inaendelea na ukatili wake bila kuzingatia maadili ya kibinadamu au kisheria, ina imani potofu kwamba inaweza kuzuia ukweli kufichuliwa kupitia mashambulio yake ya mfumo dhidi ya wanahabari,” alisema Burhanettin Duran, Mkuu wa Mawasiliano wa Uturuki, kupitia mtandao wa X.
Marekani
Rais wa Marekani Donald Trump alionyesha kutoridhishwa kwake na mfululizo wa mashambulio ya Israeli dhidi ya hospitali ya Nasser Gaza.
“Sifurahii. Sitaki kuiona,” Trump alisema kwa waandishi wa habari katika Ofisi ya Oval.
Uingereza
Katibu wa Mambo ya Nje wa Uingereza David Lammy alisema alitishiwa na mashambulio ya Israel.
“Nimeshtushwa na shambulio la Israel dhidi ya Hospitali ya Nasser. Raia, wafanyakazi wa huduma za afya na wanahabari wanapaswa kulindwa. Tunahitaji kusitisha mapigano mara moja,” Lammy alisema kwenye mtandao wa X.
Hispania
Hispania ilikashifu shambulio la Israel, ikiuita ni ukiukaji wa “dhahiri” na usio ruhusiwa chini ya sheria za kibinadamu.
“Serikali ya Hispania inalaani shambulio la Israeli dhidi ya Hospitali ya Nasser Gaza, ambalo limesababisha vifo vya wanahabari wanne na raia wasio na hatia,” Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo ilisema katika taarifa.
Ujerumani
Ujerumani ilishtushwa kwa kuuliwa kwa wanahabari, wafanyakazi wa uokoaji, na raia wengine.
“Shambulio hili lazima lichunguzwe,” wizara ya mambo ya nje ilisema kwenye mtandao wa X, na pia kuitaka Israel “kuruhusu mara moja vyombo huru vya habari vya kigeni kupata taarifa na kulinda wanahabari wanaofanya kazi Gaza.”
Italia
Waziri wa Mambo ya Nje wa Italia Antonio Tajani alisema Israel lazima ihakikishe usalama wa wanahabari Gaza.
“Kuhusu vyombo vya habari Gaza, tumeshapitisha waraka pamoja na nchi nyingine nyingi. Msimamo wetu juu ya uhuru wa waandishi wa habari haukubadilika,” alisema Tajani, akirejelea tamko la pamoja la wiki iliyopita la nchi 27.
Ufaransa
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alielezea mashambulio ya Israeli kuwa “hayavumiliki” na kuitaka Tel Aviv kuheshimu sheria za kimataifa.
Umoja wa Mataifa
Msemaji wa Umoja wa Mataifa alielezea mashambulio ya Israeli kuwa “ya kutisha kabisa.”
“Ni ya kutisha kabisa,” Olga Cherevko, msemaji wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Mambo ya Kibinadamu (OCHA), aliiambia shirika la habari la Anadolu.
Alisema kuona picha za shambulio kwenye skrini “haikubaliki,” akiashiria mashambulio mengine ya awali dhidi ya hospitali.
Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa ilisema “kuuawa kwa wanahabari Gaza kunapaswa kuudhi ulimwengu” na kusababisha ombi la haki badala ya ukimya.
Ravina Shamdasani, msemaji wa ofisi hiyo, alisema kwa taarifa ya maandishi kuwa vifo vya wanahabari katika eneo hilo vinaonyesha umuhimu wa haraka wa kuwajibishwa.
Mkurugenzi Maalum wa Umoja wa Mataifa kwa Mikoa ya Palestina iliyokaliwa, Francesca Albanese, aliwataka mataifa kuchukua hatua za haraka kuzuia “kufurika kwa damu” huko Gaza.
Jumuiya ya OIC
Jumuiya ya ushirikiano wa mataifa ya kiislamu (OIC) imelaani kuuawa kwa wanahabari na wafanyakazi wa vyombo vya habari na Israel Gaza kama “uovu wa kivita” na “shambulio dhidi ya uhuru wa waandishi wa habari.”
Umoja wa Ulaya
Kamishna wa Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen ameitaka Israel kuacha kuuwa watu “wanaojaribu kuambia dunia kinachoendelea Gaza.”
Wanahabari Wasio na Mipaka
Shirika la Wanahabari Wasio na Mipaka (RSF) limelaani vikali mashambulio ya Israel, likitaka hatua za haraka za Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuzuia mauaji haya.
Shirika hilo la habari la kimataifa limesema wanahabari watano wa Palestina walilengwa “kwa makusudi” na jeshi la Israel.