Juhudi za uokoaji zinaendelea katika mgodi mmoja nchini Tanzania uliotititia siku tatu zilizopita, na kuwafukia watu wasiopungua 25, Rais wa nchi hiyo Samia Suluhu Hassan alisema siku ya Alhamisi.
Ajali hiyo ya Jumatatu ilitokea wakati ukarabati ukiendelea katika mgodi wa Nyandolwa Mkoa wa kaskazini magharibi wa Shinyanga, karibu kilomita 200 kaskazini mwa mji mkuu, Dodoma.
Katika taarifa kwenye mtandao wa X, Rais Samia alisema "Ndugu zetu 25 waliokuwa wakifanya kazi kwenye mgodi wallifukiwa na kifusi."
Alielezea "masikitiko yake makubwa" kuhusu ajali hiyo, na kusema kuwa vikosi vya ulinzi na usalama vitasaidia katika shughuli za uokoaji "kuharakisha operesheni inayoendelea."
Ajali mbaya
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mboni Mhita amewataka watu kuwa na subira.
"Hakuna mtu alitarajia hili kutokea, naomba tuwe watulivu na tuendelee kuunga mkono juhudi za uokoaji," alisema katika eneo la tukio.
"Waliofukiwa kwenye kifusi walikuwa wanafanya ukarabati kwenye mgodi huo," alisema.
Mwezi Januari mwaka jana, wachimba migodi 22 walifariki kutokana na maporomoko katika mgodi mwingine wa dhahabu kaskazini mwa nchi, baada ya mvua kubwa kunyesha.
Na mwezi Januari 2017, watu 15 waliokolewa baada ya kukwama chini ya ardhi kwa siku mbili baada ya mgodi kutitia.